Mwenyekiti wa Chama Cha Tanzania Labour Party (TLP), Augustine Mrema, pichani, amechaguliwa na mkutano Mkuu wa Kituo cha Demokrasia nchini (TCD), kuwa Mwenyekiti mpya atakayekiongoza kwa mwaka mmoja.

Uchaguzi huo ulifanyika mwishoni mwa wiki na wajumbe wapatao 25 ambapo Mrema alipita bila kupingwa na kupewa nafasi hiyo baada ya mtangulizi wake, James Mbatia, kutoka NCCR-Mageuzi kumaliza muda wake.

Katika mkutano huo uliofanyika jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa UDP, John Cheyo, alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa kituo hicho.

Akizungumza muda mfupi baada ya kuchaguliwa, Mrema alisema amefarijika kuwa bosi katika kituo hicho kinachoundwa na vyama sita vyenye wawakilishi bungeni kikiwamo Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama cha Demokrasia na Maendeleo, TLP, Chama cha Wananchi (CUF), NCCR-Mageuzi na UDP.

Aidha, Mrema alisema yeye na viongozi wenzake wataendeleza yale yote yaliyofanywa na watangulizi wao kwa lengo moja la kujenga siyo kubomoa.

0 comments:

Copyright © 2012 KARINGA NEWS Tz